WIZARA YATOA ELIMU YA KUPUMZISHA ZIWA TANGANYIKA

Imewekwa: Sunday 31, March 2024

WIZARA YATOA ELIMU YA KUPUMZISHA ZIWA TANGANYIKA

Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza kutekeleza shughuli za upumzishaji ziwa Tanganyika mkoani Kigoma kuanzia Mei 15, 2024 hadi Agosti 15, 2024 kwa kutoa elimu kwa madiwani na watendaji wa serikali mkoani Kigoma, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa Abdallah Ulega.

Akizungumza wakati wa kikao cha kujadili utekelezaji wa upumzishwaji wa shughuli za uvuvi wa ziwa Tanganyiaka, leo machi 27, 2024 mkoani Kigoma, Mkuu wa wilaya ya Kigoma ambaye ndio mgeni rasmi kwenye kikao hicho, Mheshimiwa Salum Kalli, alisema zoezi hili ni sehemu ya kukuza Sekta ya uvuvi nchini, hali itakayosaidia ongezeko la samaki na soko katika siku za usoni kutokana na uwepo wa samaki za kutosha.

Mheshimiwa Kalli, amesisitiza juu ya umuhimu wa zoezi hilo katika ziwa Tanganyika ikiwa ni kitovu cha mazao ya samaki kutokana na mazalia kuwa mengi na yenye kukidhi mahitaji ya watumiaji.

“Ninawataka madiwani wote mpokee elimu hii ya ufugaji wa samaki kupitia vizimba na kuhakikisha mnakuwa mabalozi wa kupeleka elimu hii kwa jamii katika maeneo yenu” amesema Mheshimiwa Kalli

Naye, mwakilishi wa mkurugenzi wa Uvuvi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bwana Ambakisye Simtoe, ambae ni Afisa Uvuvi Mkuu wa Wizara, amewataka wadau wa masuala ya uvuvi kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha juu ya kupumzishwa kwa ziwa jambo ambalolitachochea ongezeko la samaki katika ziwa hilo.

Simtoe, ameeleza kuwa kwa sasa serikali ipo katika kampeni ya kutoa elimu juu ya kupumzishwa kwa ziwa hil, na nchi zote zinazohusika na usimamizi wazi wa Tanganyika tayari zimeshakubaliana kukamilisha zoezi hilo.

Simtoe ameongezea kuwa, Wizara imejipanga kuanzisha ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba kama shughuli mbadala itakayo wasaidia wananchi kumudu maisha wakati shughuli za uvuvi zikiwa zimesitishwa katika ziwa Tanganyika.

“Wananchi wamehamasishwa na utafiti umefanyika kuwa samaki wanakua vizuri wakiwa ndani ya visimba, na mpaka sasa Wizara tumeshapokea maombi kadhaa ya wananchi kwa ajili ya kuanzisha ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba, na maombi hayo yameshachakatwa na serikali mpaka sasa inaendelea kutengeneza vizimba vya kutosha jijini Mwanza na vipo tayari kwa ajili ya kusafirishwa na kuletwa Kigoma ili shughuli za ufugaji wa vizimba kuanza mara moja” amesema Simtoe

Diwani kata ya Matendo, Bwana Ilack Ramadhani ameiomba serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuharakisha Uvuvi wa vizimba mkoani Kigoma, utakao wawezesha wananchi kuendelea kupata mazao ya samaki kwa ajili ya kitoweo na shughuli za kibiashara.

Vilevile, Mkuu wa Kitengo cha Uvuvi Halmashauri ya Kigoma, BwanaYasini Tinganya amesema wamejipanga kimkamilifu kufikia malengo na kushirikisha jamii kwa kila mwalo uliopo mkoa wa Kigoma.

Pia, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Kigoma, Bwana Mayunga Kahena ameishukuru serikali kwa hatua hiyo kwani amesema italeta faida kwa ziwa Tanganyika kutokana ukweli wa kupungua samaki katika ziwa Tanganyika ambao wamepungua kwa kiasi kikubwa.

“Wananchi wa Kigoma kwa sasa wanashindwa kununua dagaa wa Kigoma kutokana na gharama kuwa kubwa sana, na nafikiri kuwa hatua hiyo itakuwa suluhisho tosha kwa kusimamisha shughuli za Uvuvi ziwa Tanganyika ili kuongeza uwezekano wa samaki katika ziwa Tanganyika”. Alisema Bwana Kahena.

.