Kuhusu Sekta ya Uvuvi

Tanzania imebahatika kuwa na maeneo mengi ya maji baridi na maji ya bahari ambapo shughuli za uvuvi hufanyika. Eneo la maji baridi linajumuisha maziwa makuu matatu ambayo ni Ziwa Victoria lenye ukubwa wa kilometa za mraba 68,800 ambapo Tanzania humiliki kilometa za mraba 35,088 (51%); Ziwa Tanganyika lenye kilometa za mraba 32,900 ambapo Tanzania humiliki kilometa za mraba 13,489 (41%) na Ziwa Nyasa lenye kilometa za mraba 30,800 na Tanzania humiliki kilometa za mraba 5,760 (18.51%). Pia, kuna maziwa ya kati na madogo, mabwawa ya asili, mito na maeneo oevu.

Eneo la Bahari limegawanyika katika Maji ya Kitaifa (Territorial Sea) yenye ukubwa wa kilometa za mraba 64,000 na Ukanda wa Uchumi wa Bahari (Exclusive Economic Zone - EEZ) wenye ukubwa wa kilometa za mraba wa 223,000. Vilevile, Tanzania Bara ina Ukanda wa Pwani wenye urefu wa kilometa 1,424 (kutoka mpakani mwa Nchi ya Kenya kwa upande wa Kaskazini na Nchi ya Msumbiji kwa upande wa Kusini). Aidha, uwepo wa ardhi kubwa ya Tanzania yenye ukubwa wa Kilometa za mraba 945,087 pamoja na rasilimali hiyo ya maji ni muhimu kwa shughuli za uvuvi na ukuzaji viumbe maji.

Sekta ya Uvuvi ni miongoni mwa sekta muhimu za kiuchumi inayochangia kukuza uchumi na kuondoa umasikini. Sekta hii imegawanyika katika tasnia za uvuvi kwenye maji ya asili na ukuzaji viumbe maji. Tasnia hizo ni muhimu katika kutoa ajira, kipato, chakula na lishe bora pamoja na kukuza Pato la Taifa. Katika mwaka 2021, sekta ilichangia asilimia 1.8 katika Pato la Taifa na ilikua kwa asilimia 2.5.

Katika mwaka 2020/2021, sekta imetoa ajira za moja kwa moja kwa wavuvi wapatao 194,804 na wakuzaji viumbe maji 31, 998 na zaidi ya Watanzania milioni 4.5 wameendelea kupata mahitaji yao ya kila siku kutokana na shughuli mbalimbali zikiwemo kuunda na kutengeneza boti, kushona nyavu, biashara ya samaki na mazao ya uvuvi pamoja na Baba na Mama lishe. Pia, sekta ya uvuvi huchangia katika usalama wa chakula nchini ambapo samaki huchangia takriban asilimia 30 ya protini inayotokana na wanyama.

Kwa upande mwingine, Tanzania Bara ina fursa kubwa katika ufugaji wa samaki ambayo bado haijatumika kikamilifu. Uwepo wa maji (maji baridi na bahari), ardhi, mfumo wa kisheria unaounga mkono ufugaji wa samaki na hali ya hewa inayofaa ni vitu vinavyovutia uwekezaji. Licha ya kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa ufugaji wa samaki, sekta ndogo haitoi mchango mkubwa katika maendeleo ya uchumi wa taifa hasa kwasababu ya ukosefu wa mbegu bora na malisho ya bei nafuuya samaki, mbinu duni za usimamizi wa ufugaji wa samaki, na mtaji. Uzalishaji wa sasa wa samaki wanaofugwa ni tani 18,717 (chini ya 4% ya jumla ya uzalishaji wa samaki) ni mdogo sana. Hivyo, juhudi za pamoja zinahitajika ili kuendeleza ufugaji wa samaki kwa kiwango kinachohitajika ili kuziba pengo kati ya mahitaji na usambazaji.

Serikali inaendelea kuwajengea uwezi wavuvi na wafugaji wa samaki ili waongeze uzalishaji na kwa kufanya hivyo ajira zitazalishwa, usalama wa chakula, kuongeza kipato cha wavuvi na watu waliopo kwenye mnyororo wa thamani pamoja na kuongeza change wa sekta ya uvuvi kwenye pato la taifa.

Kwa sasa Tanzania ina mfumo thabiti wa kisheria na kisera wa utafiti na maendeleo ya ufugaji wa samaki. Hata hivyo, vyombo hivi vya kisheria havijatumiwa kikamilifu kufikia maendeleo yanayohitajika. Kuna taasisi kadhaa za utafiti na mafunzo, pamoja na Vituo vya Ukuzaji wa Kilimo cha Majini ambavyo vikitumiwa kikamilifu, vinaweza kutoa mchango mkubwa katika utafiti, usimamizi, mafunzo na ugani. Kwa kuzingatia uwezo na fursa zilizopo, ni sharti serikali na wadau wengine waongeze juhudi zao za kukuza na kuendeleza ufugaji wa samaki.

.