HEKTA ELFU 20 ZATENGWA KWA VITALU RANCHI YA RUVU

Imewekwa: Saturday 04, July 2020

Serikali imetenga hekta elfu 20 katika Ranchi ya Ruvu kwa ajili ya kuwapatia wafugaji vitalu hususan vijiji vinavyozunguka ranchi hiyo iliyopo wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani ikiwa ni sehemu ya kutatua migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji.

Akizungumza mara baada ya kutembelea vijiji vya Fukayosi na Mkenge vilivyopo katika wilaya hiyo na kukagua eneo la mipaka ya vijiji hivyo na ranchi ya Ruvu inayosimamiwa na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO), Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema maeneo hayo yaliyotengwa watapatiwa wafugaji wenye uhitaji kwa utaratibu maalum utakaowekwa na NARCO pamoja na serikali ya wilaya ya Bagamoyo.

Naibu Waziri Ulega ameutaka uongozi wa NARCO ambao umesema kuanzia Julai 15, 2020 wataanza kupokea maombi kwa wafugaji wenye uhitaji wa vitalu katika ranchi hiyo na kutaka wafugaji kutoingiza mifugo katika mashamba ya wakulima kwa kuwa serikali inatoa maeneo hayo ili kuondoa migogoro ya ardhi.

Kuhusu uhaba wa maeneo katika wilaya ya Bagamoyo, Naibu Waziri Ulega amewataka watu waliopatiwa maeneo makubwa katika wilaya hiyo kuyaendeleza, hii ni baada ya kubaini uwepo wa maeneo makubwa katika vijiji vya wilaya hiyo ambayo hayajaendelezwa na kuwafanya wakulima na wafugaji katika maeneo hayo kukosa sehemu ya kulima na kufuga.

Awali wananchi hao walimweleza Naibu Waziri Ulega kero kubwa waliyo nayo kuwa ni uhaba wa ardhi unaopelekea wafugaji kukosa malisho na kulisha mifugo yao katika mashamba ya wakulima na kusababisha migogoro isiyokwisha.

.