KAMATI YAPITISHA MPANGO NA BAJETI YA WIZARA YA MIFUGO NA UVUVI 2026-2027
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Deodatus Mwanyika, imeridhia randama ya mpango wa bajeti ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya ( Mifugo na Uvuvi) kwa mwaka wa fedha 2026/2027, leo Machi 28, 2026 , Bungeni jijini Dodoma.
Katika michango yao, wajumbe wa kamati hiyo wameonesha kuridhishwa na vipaumbele vya wizara kwa mwaka fedha 2026/2027 licha ya bajaeti yake kuwa ndogo, huku wakiipongeza Wizara hiyo kwa maono mapana yanayolenga kukuza sekta ya mifugo na uvuvi na kwamba kamati hiyo imeahidi kuendelea kuishauri serikali kuongeza bajeti kwa ajili ya sekta hizo za uzalishaji.
Pamoja na pongezi hizo, Kamati imetoa miongozo na ushauri wa kimkakati unaolenga kuimarisha sekta za mifugo na uvuvi hususan kuongeza uzalishaji, kuongeza maeneo ya malisho ya mifugo, udhibiti wa utoroshaji wa mifugo na usimamizi wa mazao ya uvuvi, ujenzi wa bandari,na viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa ameieleza kamati hiyo kuwa katika Mwaka wa Fedha 2026/ 2027 wizara inaomba kutumia kiasi cha Shilingi Bilioni 433.4 kwa ajili ya mishahara, matumizi mengineyo na miradi ya maendeleo ya sekta za mifugo na uvuvi.
“ Mheshimiwa mwenyekiti katika mwaka wa fedha 2026/ 2027, wizara inaomba kutumia shilingi bilioni 433, 379,125,000 ambapo kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 98,279,420,000 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida (OC) na shilingi bilioni 335,099,705,000 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo, ingawa kushuka kwa bajeti hii kutaathiri utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo wizara inaisimamia” alisema Dkt. Bashiru.
Katika mwaka 2025/2026, unaoendelea kutekelezwa, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Fungu 99) iliomba kutumia jumla ya shilingi 476,655,072,000 kati ya fedha hizo, shilingi 101,516,670,000 zilikuwa ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shilingi 375,138,402,000 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.