Nifanyeje?
- Zipi sifa za kuorodheshwa kama msaidizi wa mtaalam wa mifugo? (Enlisted Paraprofessional Assistant)
- Zipi sifa za kujiandikisha kama mtaalam msaidizi wa mifugo? (Enrolled Paraprofessional).
- Daktari wa mifugo asiye mtanzania (Foreigner) anasajiliwa vipi na Baraza.
- Daktari wa mifugo asiye Mtanzania anaweza kusajiliwa na kufanyakazi hapa nchini? (Temporary and permanent registration)?
NDEGE NYUKI YAANZA RASMI KUWASAKA WAVUVI HARAMU ZIWA VICTORIA

Na Edward Kondela - WMUV, Mwanza
Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa mara ya kwanza imenunua na kuzindua matumizi ya ndege nyuki (drone) itakayofanya kazi ya kuimarisha usimamizi wa shughuli za uvuvi katika Ziwa Victoria.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ndege nyuki hiyo jijini Mwanza Aprili 13, 2025 kwa niaba ya Mgeni Rasmi Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, Naibu Waziri wa wizara hiyo Mhe. Alexander Mnyeti amesema serikali imeamua kuchukua hatua madhubuti za kisasa kuhakikisha inadhibiti uvuvi haramu kwa kutumia teknolojia ya kisasa.
Mhe. Mnyeti ameongeza kuwa katika awamu hii wizara imetumia kiasi cha Shilingi Milioni 259, kwa ajili ya ununuzi wa ndege nyuki, kutoa mafunzo kwa waendeshaji, kufunga vituo vya kudhibiti, kufanya usajili na kuanzisha mfumo wa kuhifadhi na kuchambua taarifa zinazopatikana kutoka kwenye ndege hiyo.
“Ndege nyuki hii ni kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa shughuli za uvuvi katika Ziwa Victoria. Ndege nyuki hii ina uwezo wa kukimbia kwa mwendo kasi wa Kilometa 108 kwa saa na uwezo wa kuchukua picha za matukio kutoka umbali mita 350 na kuruka mita 120 kutoka usawa wa bahari na kusafiri umbali wa Kilometa 400 na kuweza kukaa angani kwa muda wa saa mbili.” amesema Mhe. Mnyeti
Aidha, amesema mpango wa matumizi ya ndege nyuki hautaishia Ziwa Victoria pekee, bali kupeleka matumizi hayo katika Ziwa Tanganyika na Nyasa, pamoja na maeneo ya Pwani ya Bahari ya Hindi ili kuhakikisha kila pembe ya nchi inaonja matunda ya teknolojia ya kisasa katika usimamizi wa rasilimali.
Pia, amesema ndege nyuki hiyo ina uwezo wa kutoa taarifa kulingana na muda halisia na kwamba itasaidia kupunguza vitendo vya uvuvi haramu na gharama za uendeshaji wa doria ziwani pamoja na kutumika katika masuala ya utafutaji na uokoaji.
Amefafanua kuwa ndege nyuki hiyo ni kifaa cha kisasa kinachoruka angani bila rubani kwa lengo la kusaidia kuimarisha doria na usimamizi wa rasilimali za uvuvi na kuwa kifaa hicho ni mali ya serikali, wizara itaendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na taasisi zingine za serikali kuimarisha ulinzi na usalama kwenye Ziwa Victoria.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Uvuvi) Dkt. Edwin Mhede akizungumza katika hafla hiyo amesema uwepo wa ndege nyuki unaenda sambamba na takwa la kidunia la matumizi ya teknolojia rafiki za kimazingira.
Ameongeza kuwa katika mapambano ya uvuvi haramu serikali ililazimika kutumia boti na magari yanayotumia mafuta ya diesel ambayo yanaleta hewa ya ukaa kwa kiasi kikubwa ila kwa matumizi ya ndege nyuki, itakuwa ikienda eneo mahsusi ambalo kuna viashiria vya uvuvi haramu hivyo kupunguza matumizi ya boti na magari kwa ajili ya kuwasaka wavuvi haramu.
Kufuatia maelekezo ya Naibu Waziri Mhe. Mnyeti, katika kudhibiti uvuvi haramu Dkt. Mhede amebainisha kuwa atahakikisha anasimamia maelekezo hayo yakiwemo ya baadhi ya maafisa uvuvi kutuhumiwa kushiriki katika matukio ya uvuvi haramu.
Akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mhe. Amina Makilagi amesema mkoa huo unategemea sana Sekta ya Uvuvi katika kukuza uchumi, hivyo kuzinduliwa kwa ndege nyuki kwa matumizi ya kudhibiti upotevu wa rasilimali za uvuvi kutasaidia kuwabaini wahalifu na kukomesha uvuvi haramu.
Amesema kama mkoa wamekuwa wakihakikisha doria zinafanyaika mara kwa mara ili kuhakikisha maeneo yote ya Ziwa Victoria katika Mkoa wa Mwanza yanakuwa salama dhidi ya uvuvi haramu.
Baadhi wakazi wa jiji la Mwanza waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa ndege nyuki kwa ajili ya kudhibiti uvuvi haramu, wamepongeza jitihada za serikali na kusema ni jambo la kipekee kuwa na kifaa hicho ambacho wameshuhudia namna kinavyofanya kazi kwa mara ya kwanza baada ya uzinduzi.
Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeweka wazi kuwa katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2026 itatenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa ndege nyuki zaidi ili kuongeza wigo wa kudhibiti uvuvi haramu katika maeneo mbalimbali nchini.