BOTI 11 ZAKABIDHIWA KULINDA RASILIMALI ZA UVUVI ZIWA TANGANYIKA
BOTI 11 ZAKABIDHIWA KULINDA RASILIMALI ZA UVUVI ZIWA TANGANYIKA
Imewekwa: 14 May, 2025

Mradi wa FISH4ACP unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya na Serikali ya Ujerumani na kutekelezwa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) katika Ukanda wa Ziwa Tanganyika, umekabidhi Boti 11 za Doria kwa Serikali kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi zenye thamani ya Dola za Kimarekani 200,000 sawa na shilingi za Kitanzania milioni 539,834,000 ili kuimarisha usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi katika Ziwa Tanganyika
Akizungumza katika hafla ya kukabidhiwa Boti hizo kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, leo Mei 13, 2025 Mkoani Kigoma, Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma, Ndg. Hassan Rugwa amesema upatikanaji wa Boti hizi utaimarisha ushiriki wa jamii za wavuvi katika Ulinzi na Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi na hivyo kuwa na uhakika wa uendelevu wa Rasilimali za Uvuvi.
"matokeo haya tunayoyaona leo ni muendelezo wa Juhudi madhubuti za Serikali ya awamu ya Sita ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kukuza Diplomasia ya Uchumi kwa kuimarisha ushirikiano wa Kimataifa na washirika wa Maendeleo katika kuinua kipato cha wananchi, kuimarisha Usalama wa chakula na kuchochea maendeleo ya Uchumi wa jamii na Taifa kwa ujumla." amesema Ndg. Rugwa
Aidha, Ndg. Rugwa amesema Boti hizi zilizokabidhiwa leo kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, zitakabidhiwa kupitia utaratibu maalumu wa Serikali kwenye Vikundi vya Usimamizi Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMU), ikiwemo Kibirizi (Manispaa ya Kigoma), Kagunga, Mtanga (Kigoma Vijijini), Mwakizega, Kabeba, (Uvinza), Utinta, Kabwe (Nkasi), Samazi, Kipwa, Kasanga (Kalambo), pamoja na Kituo cha Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi Kigoma (FRP).
Vilevile, Ndg. Rugwa ameishukuru FAO kupitia Mradi wa FISH4ACP, pamoja na Umoja wa Ulaya na Serikali ya Shirikisho la Ujerumani kwa niaba ya Serikali kwa kutoa ufadhili wa Boti hizi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uvuvi Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Mohamed Sheikh, amesema hali ya Uvuvi kwa sasa hivi ipo vizuri, na Serikali imeendelea kuimarisha Biashara ya Mazao ya Uvuvi katika soko la ndani na nje ya nchi, na Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha Rasilimali za Uvuvi zinasimamiwa kwa njia endelevu, ili ziweze kuwanufaisha wananchi na Taifa kiujumla.
Pia, Prof. Sheikh amesema Wizara imeendelea kuimarisha Usimamizi wa maeneo ya mazalia na makulio ya Samaki katika maeneo mbalimbali ikiwemo Ziwa Tanganyika, na kwa upande wa Ziwa Victoria maeneo muhimu ya mazalia na makulia ya Samaki yameainishwa kwa ajili ya kuweka maboya ili kudhibiti shughuli za Uvuvi na uharibifu wa Mazingira kwenye maeneo hayo.
Prof. Sheikh amesema katika kukabiliana na vitendo vya Uvuvi haramu nchini, Wizara imeanza kutumia Teknolojia ya kisasa ambapo tayari imenunua ndege nyuki 1 kwa ajili ya kuimarisha mifumo ya Ufuatiliaji wa vyombo vya Uvuvi na wavuvi, na Serikali imeshatoa Boti 68 za Doria, gari 20 na pikipiki 13 kwa Vituo vya Ulinzi wa Rasilimali za Uvuvi kwa lengo la kudhibiti Uvuvi haramu na kulinda mazalia na makulio ya Samaki.
Halikadhalika, Prof. Sheikh amewataka wavuvi kutojihusisha na uharibifu wa Rasilimali za Uvuvi, na kushirikiana katika kutokomeza Uvuvi haramu.
Naye, Mratibu wa Mradi wa FISH4ACP, Bw. Hashim Muumin, akizungumza kwa niaba ya Mwakilishi Mkaazi wa FAO, amesema FAO kupitia Mradi wa FISH4ACP limeabidhi Boti hizo ili kusaidia ulinzi shirikishi wa rasilimali za uvuvi, hii ni katika juhudi za kusaidia utekelezaji wa Mpango Mkuu wa Uvuvi na Mkakati wa Hiyari wa Usimamizi wa Uvuvi Mdogomdogo (SSF Guidelines).
Bw. Muumin, amesema huu ni muendelezo wa kuzipatia nyenzo vikundi vya Ulinzi Shirikishi ili viweze kushiriki kimamilifu katika Ulinzi na Usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi, baada ya kupata Mafunzo ya mwaka jana juu ya usimamizi wa Rasilimali za Uvuvi na Ulinzi shirikishi na Shirika linaahidi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha changamoto za Uvuvi zinapungu bila ya kumsahau yeyote.