WADAU WAHIMIZWA UMOJA UTUNZAJI RASILIMALI ZA UVUVI

Ikiwa ni siku ya pili ya warsha ya kujadili ujumuishwaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa rasilimali za uvuvi wadau wa maendeleo ya sekta ya uvuvi wamehimizwa kuwa na nguvu za pamoja zitakazosaidia kulinda na kutunza rasilimali za bahari na vyanzo vingine vya maji kwa ajili ya shughuli za uvuvi.
Hayo yameelezwa Oktoba 8, 2025 katika Hoteli ya Giraffe Jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Dkt. Charles Mhina ambapo amesema serikali na wadau wengine wa maendeleo waweke jitihada za pamoja katika utunzaji wa mazingira ya viumbe maji itasaidia kuwa na uvuvi endelevu na kuinua uchumi wa jamii.
Amehimiza washiriki wa warsha hiyo kutumia jukwaa hilo ili kubadilisha mtazamo kuhusu utunzaji wa mazingira ya bahari, vyanzo vya maji na rasilimali za uvuvi ili jamiii iweze kunufaika na sekta ya uvuvi endelevu na kuondokana na umaskini.
Aidha, Katika siku ya pili ya warsha hiyo majadiliano mbalimbali yamefanyika yakiwa na lengo la kuja na mpango mkakati utakaosaidia kufanya ujumuishaji wa masuala ya bioanuwai katika usimamizi wa sekta ya uvuvi.